WASIFU WA ENOCK ATTA AGYEI ,MGHANA WA AZAM FC




Enock Atta Agyei akiwa Azam FC.
 
Enock Atta Agyei alianza kuonyesha kipaji chake akiwa na umri wa miaka sita tu, akianzia kucheza katika timu ya vijana ya King Solomon inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Ghana mwaka 2005.


Kipaji chake kikubwa cha kusakata mpira, kilimfanya akibebe kikosi cha Shule ya Msingi Effiduase Presby aliyokuwa akisoma, ambacho kilifuzu ngazi ya kanda na baadaye mkoa katika michuano ya shule nchini humo.


Enock Atta Agyei akiwa Medeama fc ya Ghana.

Mara baada ya michuano hiyo, Agyei alikuwa ni miongoni mwa nyota 26 waliochaguliwa kujiunga na Chuo cha Taifa Michezo nchini humo, wote wakipendekezwa kuingia katika academy ya chuo hicho.


Kujitoa kwake na kufanya kazi kwa bidii kulimfanya apandishwe haraka kutoka timu ya vijana chini ya umri wa miaka 12 hadi 17 kabla hajajiunga na Windy Professionals.


Nyota ya kinda huyo ilizidi kung’ara mwaka jana wakati alipoichezea msimu wa mwisho Windy Professionals na hii ni baada ya kuchangia mabao 24 yaliyofungwa na timu hiyo msimu uliopita, akifunga mwenyewe 17 na kutoa pasi za mwisho saba ndani ya mechi 29 alizocheza.


Mafanikio yake hayo yalimfanya azawadiwe Tuzo ya Mchezaji Bora anayetabiriwa kutikisa baadaye (GN Bank Award), hii ikiwa ni kwa msimu 2015-2016  wa Ligi Daraja la Kwanza Ghana wakati akiichezea Windy.


Desemba mwaka jana, haikushtua kusikia Medeama FC ya huko ikinasa saini yake, ambayo amefanikiwa kuiongoza kufika hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika kabla ya wiki iliyopita kutua Azam FC.


Kinda huyo mbali na kutokuwa na uzoefu wa mikikimikiki ya Ligi Kuu, tayari ameshawahi kuitwa katika timu za Taifa za vijana za Ghana, akianzia ya chini ya miaka 17 na sasa akiwa kwenye kile cha chini ya miaka 20.


Licha ya kutocheza hata mechi moja mpaka sasa akiwa na U-20 ya Ghana, Agyei alikuwemo katika kikosi cha timu hiyo kilichotolewa na Senegal kwa jumla ya mabao 3-2 kwenye mechi za kufuzu fainali za Mataifa ya Afrika kwa Vijana wa umri huo zitakazofanyika Zambia mwakani.


Hivi sasa , Azam FC  ndio imefanikiwa kunasa saini ya Enock Atta Agyei, ambaye tayari amesaini mkataba wa miaka miwili, huku ikimbidi kusubiri kuitumukia kalabu yake kwa kuwa alisajiliwa akiwa chini ya umri wa miaka 18.


Huyu ndiye kinda Mghana Enock Atta  Agyei anayetoa somo kwa vijana wa Kitanzania kuchukua hatua ya kujifunza kutokea kwake kwakuwa hakukata tamaa ya kusubili, Leo Viongozi wa soka letu na timu zetu wanajifunza nini?.



Makocha wa timu zetu za vijana na Timu ya Taifa ya Wakubwa wanatoa nafasi gani kwa vijana wetu chipukizi waliopo nchini na waliopo nje ya nchi kuja kuwekeza kwenye soka letu?.
TAG